Na Mwandishi wetu,Katavi
Wakufunzi waliopatiwa Mafunzo ya sensa ngazi ya Mkoa katika Mkoa wa Katavi wametakiwa kwenda kufanya kazi hiyo kwa uzalendo na kujitoa kwa moyo lengo likiwa ni kupata taarifa sahihi za watu wanaoishi ndani ya Mkoa wa Katavi.
Akifunga Mafunzo hayo yaliyofanyika kwa siku 21 katika Ukumbi wa Idara ya Maji Manispaa ya mpanda Mkuu wa Wilaya ya Mpanda Jamila Yusuph kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mwanamvua Mrindoko amewataka wakufunzi hao wa sensa ngazi ya Mkoa kwenda kutoa Mafunzo kwa umahiri kwa makarani wa ngazi ya Wilaya ili nao wawe bora na mahiri wakati wa utekelezaji wa zoezi hilo la sensa.
Aidha amewataka wakufunzi hao kwenda kufanya kazi kwa ufanisi na uzalendo kwani kazi hiyo ni ya kujitoa na ndio itakayotoa taarifa sahihi za ugawaji wa rasilimali kwa uhalisia.
Nae Kiongozi wa Mafunzo hayo ya wakufunzi kutoka ngazi ya Taifa Joyce Msoka amewataka wakufunzi hao kwenda kufanya kazi hiyo kwa uzalendo na kusisitiza Mipango ya kimaendeleo itatokana na takwimu sahihi za sensa ya watu na makazi.
Mratibu wa sensa Mkoa wa Katavi Janeth Busanya amewataka wakufunzi hao kwenda kuwafundisha makarani wa sensa ngazi ya Wilaya kwa uadilifu ili nao waweze kutekeleza kazi hiyo ya kizalendo kwa moyo.
Baadhi ya Washiriki waliohitimu Mafunzo ya sensa ngazi ya Mkoa yaliyofanyika kwa siku 21 katika Ukumbi wa Idara ya Maji Manispaa ya Mpanda Mkoa wa Katavi. |
Nao baadhi ya washiriki waliohitimu Mafunzo hayo ya kwenda kuwafundisha makarani wa Wilaya akiwepo Mariam Yasin wameishukuru Serikali kwa kuwapatia Mafunzo hayo na kuahidi kwenda kuifanya kazi hiyo kwa uzalendo kwani takwimu sahihi ndizo zitakazoleta Maendeleo kwa uhalisia.
Nae Mshiriki Florence Ngua kwa niaba ya washiriki wote ameahidi kuwa wapo tayari kufanyakazi kadri ya maelekezo waliyopewa kwa uadilifu na kuhakikisha Mkoa wa Katavi unakuwa na taarifa sahihi za watu wanaoishi ndani ya Mkoa huo.