Na George Mwigulu.
WARAKA wa elimu namba mbili wa mwaka 2021 kuhusu urejeshwaji shuleni wa wanafunzi waliokatiza masomo katika elimu ya msingi na sekondari kwa sababu mbalimbali hususani ujauzito nakuanza rasmi kutekelezwa nchini mwaka 2022 ni faraja kubwa kwa wanafunzi wa kike ambao ndoto zao zilififia na kukosa matumaini ya elimu.
Serikali ya awamu ya sita chini ya rais Samia Suhulu Hassain kwa
kutambua umuhimu wa masuala ya usawa wa kijinsia kwenye upatikanaji wa fursa ya elimu
amefanikisha urejeshwaji wa wanafunzi hao darasani na kupongezwa dunia kote
ambapo Mkoa wa Katavi unaendelea kufanikisha adhima hiyo licha ya baadhi ya
wazazi na walezi bado hawajawa na mwitikio mzuri kwa ajili ya kuwarejesha
masomoni wanafunzi wa kike.
Serikali ya Mkoa huo chini ya utaratibu wa kuboresha elimu ya
sekondari Tanzania (SEQUIP) inatekeleza mpango huo ambapo licha ya kupiga hatua
ya kuanzisha vituo vitatu vya shule na kudahili wanafunzi 71 lakini bado
matatizo yanawarudisha nyuma.
Beatrice Gati,Afisa elimu ya watu wazima Mkoa wa Katavi
amebainisha hayo hivi karibuni ofisini kwake ambapo amesema dira ya elimu
nchini ni kuwa na watu walioelimika,maarifa,stadi,uwezo na mtizamo chanya
utakaochangia kuleta maendeleo kwa kila mtoto bila kujali jinsi anapata fursa
sawa ya kupata elimu bora.
Gati ameweka wazi kuwa kutokana na serikali kuongeza fursa
na kuboresha elimu kwa ngazi zote kwa kutunga sheria,kanuni,miongozo na nyaraka
lakini jamii inapaswa kuwa sehemu ya kukataa mambo yanayomrudisha nyuma
mwanafunzi hususani wa kike.
Akielezea mpango wa SEQUIP amesema wanafunzi wanaokatiza masomo
wazazi na walezi ni chanzo kikubwa cha kushindwa watoto hao kunufaika na elimu
kwani wanakosa ndugu wa kuwaachia watoto ili waendelee na masomo.
“Unakuta mzazi anasema aah!,mtoto atamwachia nani.Mimi nina
shughuli zangu za kwenda shambani na nafanya biashara…kwahiyo wanakosa walezi ambao
watakuwa waangalizi wa watoto pindi wawapo shuleni” Amesema Gati.
Wasichana kukata tamaa baada ya kupata ujauzito na ugumu wa
maisha umetajwa pia kuwa ni sababu zinazokwamisha kurejea masomoni wanafunzi
hao kwa maana baadhi yao baada ya kupata ujauzito wamelazimishwa kuolewa na
kuendelea na maisha mengine.
Afisa Elimu huyo amesema “wasichana wengi wa kike wanaopata
ujauzito wanakata tamaa kwa kuhisi wamefanya makosa makubwa,kubaguliwa na
kutengwa na wanafunzi wenzao ambapo changamoto zote hizo zinawafanya kuathirika
kisaikolojia”.
Katika kuhakikisha mpango wa kuwarejesha masomoni wanafunzi
waliopata mimba Katavi unafanikiwa. Mkoa huo umepitisha maazimio mwezi wa nane mwaka huu kuwa kila halmashauri kuanzisha kituo cha wanafunzi wa kike cha
SEQUIP na kudahili wanafunzi kuanzia 50 ambapo kwa halmashauri tano watakuwa na
wanafunzi hao zaidi ya 250 kuanzia mwezi wa kwanza mwaka ujao.
Mwl, Idrisa Meru na Mtaalamu wa masuala ya saikolojia ya
wanafunzi kutoka kituo cha Elimu ya Mfumo usio rasmi Kashato,Manispaa ya Mpanda
Mkoani hapa anadhibitisha ugumu wa kufanya vizuri kitaaluma wanaoupata wanafunzi
hao kwa sababu ya ushirikiano mbovu kati ya wazazi/walezi na waalimu uliopo.
Mwl Idrisa anasema “...Mwanafunzi mmoja wa kike alinifuata na kunieleza namna anavyobaguliwa na familia yake kutokana na kupata ujauzito kwa bahati mbaya baada ya mtoto kuzaliwa wazazi wake walimwita ni haramu lugha ambayo ilimvunja moyo msichana huyo na kuathiri mahuzulio yake darasani”.
|
Akijibu hoja ya mfumo wa elimu usio rasmi kuwa unawatenga
wanafunzi na kuonekana kama kundi maalumu amesema “Kuna faida kubwa kwenye
mfumo huu,kuliko wakosoaji wanavyofikiria,mbali na kusoma masomo ya sekondari
waliyokatisha,wanafundishwa masuala mengine yatakayowapa ujuzi na kuendesha
maisha yao na kulea watoto wao huku ikiwa ni sehemu nzuri ya kuepuka kubaguliwa
na wanafunzi wengine wasio na watoto na kuwaathiri kisaikolojia” Amebainisha
Mwl Idrisa.
Kwa upande wa mwanafunzi wa kike wa kituo cha Elimu ya Mfumo
usio rasmi Kashato,Patricia Mpagama amesema zipo sababu zinawafanya wasichana
kutokurudi shule ambazo ni wazazi kukosa mwamko wa kuwapigania
watoto wa kike na badala yake kulenga kuwaozesha,kuwapa jukumu la kuwa walezi
wa watoto wa ndugu zao na mazingira mabovu ya kutokuishi na wazazi kwa sababu
ya vifo na kuwa kikwazo kwa wasichana waliopata ujauzito kutokurudi shule.
“Unakuta binti wa miaka 18 anaishi na bibi yake kwa kuwa
wazazi wake walishafariki anaogopa kumwacha bibi yake nyumbani maana yeye ni
nguzo ya kuhudumia familia bila kujali umri wake kuwa bado ni mdogo” Amesema
Patricia.
Patricia anashukuru rais Samia Suhulu Hassain kwa mpango huo
kwani anaimani atatimiza ndoto zake za kuwa daktari bingwa kwani dada yake
alishindwa baada ya kupata changamoto inayofanana na yake “Lakini mimi nahitaji
kuzitimiza kwa sababu ndoto ya kuwa daktari nilikuwa nayo tangu nikiwa mtoto
mdogo” Amesisitiza Patricia.
Charles Mabula,Mkazi wa Mtaa wa Rungwa Manispaa ya Mpanda Mkoa
wa Katavi,kama mzazi anaeleza kuwa suala la wanafunzi kukatizwa masomo hasa kwa
kupata ujauzito wazazi wengi wameshindwa kupokea na kukubali makosa
yanayofanywa na watoto wao hivyo kukata tamaa ya kuwarudisha shule kuendelea na
masomo pindi wanapojifungua licha ya serikali kuweka mfumo mpya wa kuwarejesha
shule.
Mabula amesema kuwa mfumo mpya wa elimu hiyo bado haujapewa
msukumo mkubwa kama ilivyo kwa elimu iliyo ya mfumo rasmi ambapo utaona
viongozi mbalimbali wa serikali wakitoa matamko makali ya kuhakikisha wazazi na
walezi wanaandikisha watoto shule kuingia darasa la kwanza au kidato cha
kwanza.
Ameeleza ili Mkoa wa Katavi uweze kufikia mpango huo mpya wanapaswa
kutoa hamasa kwa nguvu kwenye jamii yote ya Mkoa wa Katavi licha ya kuwa na
changamoto mbalimbali ambazo zinaweza kujitokeza kukwamisha juhudi hizo
kutokana na kuwa suala la mwanafunzi wa kike kurudi shule ni hiali yao kama
mtu anayefahamu umuhimu wa elimu au la!.