Kifo cha Rais John Magufuli: Hadithi ya rais ambaye alikabiliana na corona tofauti na dunia
Rais wa Tanzania John Pombe Magufuli akizindua mradi mkubwa wa barabara Februari 24, jijini Dar es salaam alijigamba kwa mafanikio yaliyofikiwa na chama cha mapinduzi CCM.
"Mradi ulikamilika kwa wakati kwa sababu hakuna aliyetumia corona kama kisingizio cha kucheleweha'' alisema akiwapongeza wahandisi na kuwaagiza maafisa wa serikali kutovumilia yeyote atakayetumia janga la corona kama kigezo cha kuchelewesha mradi.
Hii haikuwa na tofauti na uzinduzi uliopita ambapo alimalizia hotuba yake kwa msisitizo wa kauli mbiu yake ya HAPA KAZI TU.
"Tanzania ni tajiri,tuutumie utajiri wetu kuleta maendeleo ''alisisitiza na kuhimiza Watanzania kulipa kodi.
Siku tatu baadae Magufuli aliweza kuonekana hadharani kwa mara ya mwisho.
Tangu kuchaguliwa kwa mara ya kwanza mwaka 2015 Magufuli alijipambanua kama mtu wa vitendo, tofauti na watangulizi wake.
Namna yake ya kutekeleza majukumu ikiwemo kutumbua majipu ilimpatia mashabiki wengi ndani na nje ya mipaka ya Tanzania hususan katika ukanda wa Afrika Mashariki ambako kampeni ya #WhatWouldMagufuliDo iliibuka na kupata umaarufu kwa kusifia utendaji wake usiokuwa na simile katika mapambano dhidi ya ufisadi na kusimamia miradi ya ujenzi wa miundo mbinu bila kuchoka.
Watanzania walizingatia zaidi mtindo mashuhuri wa uongozi wa Magufuli ambao ulikuwa mfano wa kusifiwa na viongozi wengine Barani Afrika.
Kipenzi cha watu
Wafuasi wake watakosa mikutano yake ya mara kwa mara alipokuwa ziarani nchini Tanzania ambapo alisimama mara kadhaa vituoni kuzungumza na wananchi.
Ziara hizo ambazo mara nyingi ziliibua udhaifu wa watendaji wa serikali zilitangazwa mubashara katika runinga na kupata umaarufu kwa wananchi wengi kutumia fursa hiyo kuelezea matatizo yao.
Umati wa wananchi uliuzunguka msafara wa rais na kumtazama kwa karibu akiwa amezungukwa na walinzi wake waliojihami kwa silaha.
Akisimama kwenye gari yake na kutumia kipaza sauti mikononi mwake Magufuli aliwasikiliza na kuwahoji kwa kina.
Majibu yalikuwa mchanganyiko, sheria mpya ingetangazwa, au afisa angetimuliwa kibarua au kushushwa cheo au aliyeuliza swali angepuuzwa.
Wapinzani wake kisiasa mataifa jirani na makampuni ya uchimbaji madini, mataifa ya magharibi na yeyote aliyeonekana kugusa maslahi ya Tanzania alilengwa na serikali yake.
Wakosoaji wake wanasema alikuwa dikteta ambaye hakuweza kuvumilia kukosolewa, wala utani wa wasanii wa muziki ,wachekeshaji au watumiaji wa mitandao ya kijamii.
Alisababisha hofu nchini humo ambapo hata kutojulikana kwake alipo kwa zaidi ya majuma mawili sera zake tata ziliendelea kutekelezwa ikiwemo polisi kuwakamata watu waliozusha kuhusu wapi alipo rais au kuuliza yuko wapi raisi Magufuli?
Hali hii ya mambo imekuwa ikipingana na namna alivyojipambanua kama mtetezi wa utu wa Watanzania.