TAKUKURU KATAVI YAFANYA UFUATILIAJI WA FEDHA ZA UTEKELEZAJI WA MIRADI

 


Naibu Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Katavi Faustine Maijo


Na  Walter   Mguluchuma

     Katavi

Katika kipindi cha  Oktoba hadi Disemba,2021 Takukuru Mkoa wa Katavi  wamefanya ufuatiliaji  wa fedha  za  utekelezaji  wa miradi  ya Maendeleo  yenye jumla ya zaidi  ya shilingi   milioni 67.

Hayo yameelezwa na Naibu  Mkuu wa Takukuru Mkoa wa  Katavi  Faustine  Maijo wakati akitoa taarifa   mbele  ya  Waandishi wa Habari  juu ya  Utendaji kazi wa Taasisi hiyo kwa kipindi cha miezi mitatu iliyopita .

Amebainisha  kuwa katika kipindi cha miezi hiyo mitatu Takukuru  Mkoa wa  Katavi wamefuatilia miradi ya maendeleo  yenye thamani  ya shilingi  67,500,000.

Ambapo ameitaja miradi hiyo ni  umaliziaji wa madarasa  mawili  katika  shule  ya Msingi Shikizi  Halmashauri  ya Manispaa ya Mpanda wenye thamani ya  Tsh 25,000,000, Umaliziaji wa madarasa  mawili  katika  shule  ya Msingi Misunkumilo wenye thamani ya sh,2,500,000.

Na ujenzi  wa madarasa  mawili  na ofisi  moja ya walimu  katika shule ya msingi  Igalula Halmashauri ya Tanganyika  wenye thamani ya Tshs  40,000,000.

Maijo  amesema lengo la  ufuatiliaji  huo ni kuangalia  iwapo  kuna mianya ya rushwa kwenye utekelezaji wa  miradi  na kuongeza uwazi  na upatikanaji wa  thamani  ya fedha kwenye miradi  ya serikali  ili kuboresha huduma kwenye  shughuli za serikali .

Amefafanua kuwa  mapungufu machache yaliyobainika  katika ukaguzi  wa miradi  hiyo yangeweza  kusababisha  mianya ya rushwa lakini wameyafanyia kazi  kwa kufanya vikao na wadau wa miradi husika pamoja  na kuwapa elimu  kwa lengo  la kuondoa  mianya hiyo ya rushwa .

"elimu hii  itasaidia  katika kuimarisha usimamizi  wa miradi  kwa kusisitiza uzingatiaji  wa sheria  na kanuni  za manunuzi  ya umma  ili  kupata  miradi  bora  yenye kukidhi  thamani  ya fedha"alisisitiza  Maijo

Aidha katika hatua nyingine Takukuru wameweza kufuatilia  utekelezaji  wa miradi ya ujenzi  wa vyumba  vya madarasa  ya shule za  sekondari  na vituo shikizi  namba 5441 chini ya  mpango wa maendeleo  na Ustawi  wa  Taifa  na Mapambano  dhidi ya UVIKO 19 kupitia mpango huo  Halmashauri  ya Wilaya ya Mlele  ilipokea jumla ya  Tshs  680,000,000.

Katika  kusimamia  mradi huo Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mwanamvua  Mrindoko   aliunda timu  za ufuatiliaji  katika Halmashauri ya Mlele  ikiongozwa na Naibu mkuu wa Takukuru  Mkoa wa Katavi  Faustine  Maijo .

Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mwanamvua Mrindoko


Timu  hiyo iliweza kufuatilia  ujenzi wa vyumba 34 vya madarasa , madawati 360, meza 433, na viti 412 ambapo  jumla  ya kiasi cha  Tsh,100,724,838  timu hiyo iliweza kuokoa  na kupelekea Mkuu wa Wilaya ya Mlele  Filiberto  Sanga   kumtunuku  Naibu Mkuu wa  Takukuru  Cheti  cha usimamizi bora .


Mkuu wa Wilaya ya Mlele Filberto Sanga

Pia kwenye kipindi cha miezi mitatu Takukuru wameweza kupokea jumla ya malalamiko 51 huku Tamisemi na  Amcos  zikiwa zinaongoza kwa kulalamikiwa.

Naibu Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Katavi Faustine Maijo akisoma taarifa ya Utendaji kazi wa Ofisi ya TAKUKURU Mkoa wa Katavi kwa kipindi Cha miezi mitatu ambayo ni kuanzia Oktoba Hadi Disemba,2021 mbele ya Waandishi wa Habari.

Search This Blog

CHAGUA HABARI

Pages