ZAIDI YA BILIONI 8 ZATENGWA HOSPITALI YA MKOA WA KATAVI KUPITIA MPANGO WA MAENDELEO KWA USTAWI WA TAIFA NA MAPAMBANO DHIDI YA UVIKO 19

Mstahiki Meya wa Manispaa ya Mpanda Haidary Sumry alipotembelea Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Katavi inayoendelea kujengwa na Viongozi mbalimbali wa serikali ya Mkoa pamoja na Wazee Maarufu 


Na Walter Mguluchuma

Katavi

Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Katavi  kupitia mpango  wa maendeleo  kwa ustawi  wa Taifa  na mapambano dhidi ya UVIKO 19 imetengewa  kiasi cha zaidi ya shilingi bilioni 8 kwa ajili  ya uendeshaji  wa jengo  kuu la  Hospitali  na majengo mbalimbali pamoja na ununuzi wa  kipimo cha CT Scan na Digital xray.

Hayo  yameelezwa na  Mganga  Mfawidhi  wa Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Katavi  Dr  Yustina Tizeba  wakati akitoa taarifa ya maendeleo ya ujenzi wa Hositali ya Rufaa Mkoa wa Katavi inayoendelea kujengwa na kupandishwa  hadhi kuwa Hospitali ya Rufaa ya Kanda   kwa Viongozi wa Madhehebu ya dini,Wazee maarufu  na Viongozi wa Kimila  walipokuwa wameongozana na Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mwanamvua Mrindoko   kwenye ziara ya kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa ndani ya Mkoa huo.

 Alisema  Serikali  kupitia  Wizara  ya Afya  na Ofisi ya Mkoa  inaendelea kutekeleza  mradi  wa Ujenzi  wa Hospitali  ya Rufaa ya  Mkoa wa Katavi  kama ilivyoelekezwa  na Waziri  Mkuu Kasim Majaliwa  alipokuwa kwenye ziara ya kikazi Mkoa wa Katavi Agost 21 mwaka jana alipotembelea Hospitali hiyo na kutoridhishwa na kasi ya ujenzi uliokuwa ukiendelea .

Amebainisha kuwa  Hospitali hiyo  kupitia Mpango wa Maendeleo  kwa Ustawi wa Jamii wa Taifa  na Mapambano  dhidi ya UVIKO 19 imetenga kiasi  cha jumla ya  Tshs bilioni 8.5 kwa ajili  ya uendelezaji  wa Jengo  kuu la Hospitali  ambazo zimepangiwa kufanya shughuli mbali mbali kama ifuatavyo .

Ujenzi wa jengo la ICU utakaogharimu Milioni 560,Ujenzi wa Jengo la  EMD  milioni 300, Ununuzi wa vifaa tiba vya  ICU na  Emd  Tsh bilioni 1.4, Ununuzi wa  CT Scan  na  Digital  Xray Tshs Bilioni 2.6, Ujenzi wa Hospitali Bilioni 3,Nyumba ya mtumishi Tshs milioni 90,  mafunzo ya watumishi Tshs milioni 90,gari la kubebea wagonjwa na Utawala milioni 430.

Dr Tizeba ameeleza kuwa  mpaka sasa wamepokea fedha  kiasi cha Tshs Bilioni 2.6 kwa ajili ya ujenzi  wa jengo  la wagonjwa  mahututi  na jengo la wagonjwa wa dharura  pamoja na vifaa vyake  na kamati ya ujenzi  itakaa  ili kazi iweze kuanza  mara moja  na wanahakikisha watasimamia  kwa umahiri mkubwa na kwa uzalendo ili ujenzi ukamilike kwa wakati na kwa kiwango chenye ubora.

Pia Serikali imetowa  kiasi cha Tshs bilioni 5.9 kwa ajili ya  matumizi  ya ununuzi  wa vifaa tiba  kwa ajiri ya Hospitali hiyo  na tayari fedha hizo zipo bohari kuu ya dawa mara tuu ujenzi utakapo kamilika  itakuwa na uwezo  wa kuanza kazi.

Aidha Dr Tizeba aliishukuru Serikali  ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  chini ya  Uongozi  wa Rais Samia  Suluhu Hassan  kwa kuwapatia  fedha  za kuendeleza  ujenzi wa mradi  huo kwani ni imani yao mradi  ukikamilika utasaidia kuboresha  afya  kwa wana Katavi  na Taifa kwa ujumla .

Mkuu wa Mkoa wa Katavi  Mwanamvua Mrindoko  alisema kuwa lengo la Serikali  ni kuifanya hospitali hiyo kuwa ya kisasa huku mchakato wa kuifanya kuwa  ya kanda ukiendelea na haoni sababu yoyote kwa Mkandarasi Suma Jkt kushindwa kumaliza kazi kwa wakati kwani fedha zipo  na nyingine zaidi ya Bilioni 5 zimeletwa hivi karibuni.

Meya wa Manispaa ya Mpanda  Haidari Sumry amesema kukamilika kwa  hospitali hiyo kutawasaidia wakazi wa Mkoa wa Katavi ambao walikuwa wakilazimika kwenda Hospitali  za Rufaa kupatiwa matibabu  na wengine kwenda kwa ajili ya vipimo .

Na pia itakuwa ni furusa kwa wakazi wa Mkoa wa Katavi  kunufaika kwa kujiongezea kipato kwani kukamilika kwa Hospitali hiyo kutaongeza idadi ya watumishi na familia zao .

Nae  Mwenyekiti wa Mila na Destuli  Mkoa wa Katavi Michael Lusambo amezipongeza jitihada zinazofanywa  na Serikali  koboresha huduma za afya kwani ndio Msingi wa Maendeleo bila Afya imara Maendeleo yatakwama.


Kulia Mwenyekiti wa Mila na Desturi Mkoa wa Katavi Michael Lusambo akimsikiliza kwa makini Mstahiki Meya wa Manispaa ya Mpanda Haidary Sumry akieleza namna Vijana walivyonufaika kwa kupata ajira katika mradi wa Ujenzi wa Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Katavi unaoendelea  maeneo ya Rungwa.


Search This Blog

CHAGUA HABARI

Pages