SERIKALI KUWAPATIA MAAFISA UGANI WOTE NCHINI VIFAA VYA KUPIMIA UBORA WA UDONGO

 

Rais Mstaafu wa awamu ya nne Dr Jakaya Kikwete (katikati)ambae ni Mjumbe wa Bodi  ya Shirika la Kimataifala la AGRA linalojishughulisha kuinua hali ya kilimo cha wakulima wadogo katika Afrika ikiwemo na Tanzania akiwa na Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mwanamvua Mrindoko (kushoto) na Makamu wa Rais wa AGRA  Agy Konde(kulia) kabla ya kuwahutubia wananchi wa Kata ya Majimoto Halmashauri ya  Mpimbwe Mkoa wa Katavi wakati wa ziara yake ya kutembelea miradi inayotekelezwa na Shirika hilo katika Mkoa wa Katavi.


Na Walter Mguluchuma

   Katavi

Serikali kwa kupitia Wizara ya kilimo imepanga kuwapatia maafisa ugani wote nchini vifaa vya kupimia ubora wa udongo,pikipiki 2000 na elimu itakayo wasaidia wakulima wadogo na wakubwa kuweza kulima kilimo bora na cha kisasa  kitakacho wasaidia kuongeza tija  katika uzalishaji wa mazao  na kukuza uchumi wao na kuongeza pato la Taifa .

 Kauli hiyo ya Serikali imetolewa na Naibu  Waziri wa Kilimo Antony Mavunde  wakati alipokuwa akiongea na wananchi wa  Halmashauri ya Mpimbwe wakati wa ziara  ya  Mjumbe wa Bodi ya Shirika la Kimataifa la AGRA linalojishughulisha kuinua hali ya wakulima wadogo wadogo wa Afrika ikiwemo na Tanzania Rais Mstaafu wa awamu ya nne Dr Jakaya  Kikwete alipokuwa akifanya ziara katika Mkoa wa Katavi kuangalia utendaji kazi unaofanywa na shirika hilo aliyekuwa ameambatana na Naibu Waziri wa kilimo .

Alisema  Serikali  imedhamiria kuwapatia maafisa ugani wote hapa nchini elimu  ambayo itawajengea uwezo  wa kutoa elimu kwa wakulima ili waweze  kulima kilimo bora cha kisasa na kuzalisha mazao yao ziada.

 Amebainisha kuwa wamepanga kuwapatia  maafisa ugani wote vipimo  vya kupimia ubora wa udongo  ili waweze kuwasaidia wakulima kujua ubora wa udongo kwenye maeneo yao wanayolima na kuwafanya wawe na uhakika wa eneo wanalo lima lina hitaji nini.

Naibu waziri Mavunde amesema kuwa  Serikali inaupungufu wa Maafisa ugani katika mikoa yote hapa nchini kwani kuna uhitaji wa Maafisa ugani Elfu ishirini lakini waliopo sasa hawazidi  elfu sita na mia tano .

Hivyo  kwa kutambua umuhimu wa sekta ya kilimo Wizara imenunua pikipiki 2000 kwa ajili ya  kuwapatia Maafisa Ugani kwenye Mikoa yote na kwakuzingatia maeneo yenye uzalishaji mkubwa ili kuwarahisishia Maafisa ugani  kufikia wakulima kwa urahisi.

Rais Mstaafu wa awamu ya  nne ambae ni Mjumbe wa Shirika la Kimataifa la AGRA Dr Jakaya   Kikwete  amesema kuwa  shirika  la Agra  ni shirika la Kimataifa na lilianzishwa  na aliyekuwa Katibu Mkuu wa umoja wa Mataifa Kofi Anani.

Alifafanua kuwa  shirika hilo ni la kimataifa  na shabaha yake kubwa  ni kuleta  mageuzi ya kilimo kwa wakulima wadogo wa Afrika ikiwemo na Tanzania  ili kumfanya  mkulima mdogo aweze kulima kilimo bora cha kisasa na chenye tija  ili mkulima aweze kupata mazao mengi  na aweze  kuongeza kipato chake na aweze kubadili maisha yake na kukuza uchumi wa nchi.

Dr Kikwete amesema kuwa hakuna nchi inayopiga hatua  katika uzalishaji wa mazao ya kilimo bila kuwepo kwa mchango wa wakulima wadogo na ndio maana AGRA kwa kutambua umuhimu wao wameamua kuwasaidia wakulima wadogo na wala sio wakulima wakati na wakubwa.

Amesema shirika hilo kwa Mkoa wa Katavi wamefanya ukarabati wa maghala 17 ya kuhifadhia mazao na wamejenga maghala mapya mawili lengo ikiwa ni kumfanya mkulima awe na sehemu ya kuhifadhia mazao na sehemu ya kuuzia na wamekuwa wakiwasaidia wakulima kupata mbegu bora na pembejeo za kilimo .

Makamu wa Rais wa AGRA Agy  Konde  ameeleza kuwa hali ya uzalishaji wa mkulima mdogo wa Tanzania bado upo chini tofauti na nchi ya Ephiopia ambao wao Ekari moja wanazalisha tani saba za mahindi wakati Tanzania wanazalisha tani mbili .

Nae Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mwanamvua Mrindoko alisema  AGRA wamekuwa na mchango mkubwa katika kuinua sekta ya kilimo kwa kupitia wakulima wadogo na ukarabati wa maghali waliofanya umesaidia Mkoa wa Katavi kuongeza vituo zaidi vya kununulia mazao.

Rais wa Tanzania wa Serikali ya Awamu ya Nne Dr Jakaya  Kikwete ambae ni Mjumbe wa Bodi ya Shirika la Kimataifala la AGRA linalojishughulisha na maswala ya kuinua hali ya kilimo cha wakulima wadogo wa Afrika akiwemo na Tanzania akiwahutubia wananchi wa Kata ya Maji Moto Halmashauri ya Mpimbwe Mkoa wa Katavi namna ambavyo AGRA ilivyotekeleza  shughuli zake katika Mkoa wa Katavi pembeni yake  ni Makamu wa Rais wa AGRA  Agy  Konde.


Search This Blog

CHAGUA HABARI

Pages