ZAIDI YA BILIONI 9.3 SAWA NA ASILIMIA 58 ZIMEPOKELEWA NA TANROAD KATAVI KWA AJILI YA MATENGENEZO YA BARABARA BAJETI YA 2021/2022

 

Meneja wa Tanroads  Mkoa wa Katavi Mhandisi Martin Mwakabende akifafanua Jambo baada ya kusoma Taarifa ya Utekelezaji wa kazi za   Tanroads Mkoa wa Katavi mbele ya Wajumbe wa Bodi ya Barabara wa Mkoa huo.

 Na  Walter MguIuchuma

     Katavi

Ofisi ya Wakala wa barabara Mkoa wa Katavi TANROADS imepokea Jumla ya Tshs Bilioni  9.342 sawa  na asilimia 58 ya Bajeti ya Matengenezo ya Barabara za Mkoa katika mwaka wa fedha  unaoendelea  wa 2021/2022.

Hayo yameelezwa na Meneja wa Tanroads Mkoa wa Katavi Mhandisi Martin Mwakabende wakati alipokuwa akitowa taarifa ya utendaji kazi wa Tanroads wakati wa kikao cha bodi ya barabara cha Mkoa wa Katavi kilichofanyika katika ukumbi wa maji.

Ameeleza kuwa  katika mwaka wa fedha wa 2021/2022 Mkoa wa Katavi  ulitengewa  bajeti ya  Tshs  bilioni 15. 997 kwa ajili ya matengenezo  na ukarabati wa Barabara  kati ya fedha hizo  mfuko wa Barabara  ni Tshs  bilioni 12.757 na fedha za  maendeleo  ni Tshs bilioni  3.240.

Amebainisha kuwa  mapendekezo ya  bajeti ya mwaka wa fedha wa 2022/2023 wamependekeza kiasi cha jumla ya Tshs bilioni 24.61 huku  Tshs bilioni 15.708 zikiwa ni fedha kutoka mfuko wa barabara na Tshs bilioni 8.901 kutoka mfuko wa Maendeleo .

 Mwakabende ameeleza kuwa  kwa mwaka wa fedha unaoendelea  Tanroads Mkoa wa Katavi  wamesaini mikataba  28 na Wakandarasi  mbalimbali  na Miradi hiyo ipo katika hatua mbalimbali za utekelezaji  ambapo kwa ujumla  ipo  hatua ya asilimia 39.

 Amefafanua kuwa  upembuzi  yakinifu  na usanifu  wa kina  barabara   ya Mpanda   Ugala  Kaliua , Ulyankuru hadi Kahama yenye urefu wa km 457 mhandisi mshauri  amewasilisha  nyaraka  za ufanifu  kwa mwajiri ambae sasa anafanya mapitio ya mwisho na utekelezaji wake  upo asilimia 85.

Utekelezaji wa Barabara ya Kagwira hadi  Karema  yenye  urefu wa km 112 upembuzi yakinifu umefanywa  na hatua ya utekelezaji  imefikia asilimia 80.

Kuhusu Miradi ya Barabara za Kitaifa Mhandisi Mwakabende amesema kuwa  serikali imetangaza zabuni za  Ujenzi wa Barabara  kwa kiwango cha lami  katika Barabara  za  Kibaoni kuja Mpanda urefu wa km 50 na Vikonge kwenda  Luhafe  km 25 ambapo manunuzi ya miradi hiyo yote  imekamilika  na Maandalizi ya kusaini mikataba  ipo katika hatua za mwisho .

Amezitaja baadhi ya changamoto za utekelezaji wa kazi  ni utaratibu  wa kupata  msamaha wa kodi  kwa Miradi ya Ujenzi  inachukua muda  mrefu sana  hivyo kuchelewesha  utekelezaji  wa kazi  za Matengenezo ya barabara .

Changamoto nyingine ni wananchi  kufanya shughuli  za kilimo  ndani ya  maeneo  ya Uhifadhi wa barabara,uharibifu wa alama za Barabarani  na kuchelewa  kupatikana kwa  GN pia kwenye maeneo ya Barabara zinako pita hifadhi kumekuwa na tatizo kwa Wakandarasi kutoruhusiwa kuchimba vifusi kwenye  Hifadhi za Tanapa .

Mratibu wa Rarura wa Mkoa wa Katavi Inocent Mlay  ameeleza kuwa Mkoa wa Katavi bado kuna shida ya Wakandarasi kwani Wakandarasi wengi waliopo hawana vifaa vya Ujenzi wa Barabara hali inayosababisha Wakandarasi wengi kutoka nje ya Mkoa na hasa wakati wa Matengenezo ya  barabara za lami .

Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mwanamvua  Mrindoko amezitaka Tanroads na Tarura kuhakikisha barabara zote ambazo wanazisimamia zinapitika wakati wote licha ya kuwa bado mvua zinaendelea kuonyesha kwa kipindi hiki .

Amewaonya Wakandarasi ambao wamekuwa hawafanyi kazi zao vizuri kwa kutokuwepo katika maeneo yao ya kazi  Bodi ya Barabara ya Mkoa haita sita kuwachukulia hatua  na kupeleka mapendekezo kwenye mamla husika ili wafutiwe leseni zao za ukandarasi. 


Wajumbe wa Bodi ya Barabara wa Mkoa wa Katavi wakiwa kwenye kikao cha 18 cha Bodi ya Barabara kilichofanyika kwenye Ukumbi wa Idara ya Maji Manispaa ya Mpanda

Search This Blog

CHAGUA HABARI

Pages