| Picha na Mtandao |
Na Walter MguIuchuma
Katavi
Watu wawili wamenusurika kuuwawa na Tembo katika kijiji cha Migunga,Kata ya Majimoto,Tarafa ya Mamba Halmashauri ya Wilaya ya Mlele Mkoa wa Katavi.
Akitoa taarifa kwa Waandishi wa Habari Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Katavi Ali Makame Hamadi alisema kuwa waliojeruhiwa katika tukio hilo ni Michael Msasa (30) kwa kukanyagwa na Tembo pamoja na Ayubu Clement (24) aliyejeruhiwa kwa meno tumboni na Tembo huyo.
Kamanda Makame alieleza kuwa Tembo huyo alitoroka kutoka Hifadhi ya Taifa ya Katavi kwa kupitia kijiji cha Luchima na kuelekea kwenye mashamba ndipo alipowakuta majeruhi hao wakiwa shambani wanalima na kuwajeruhi.
Baada ya tukio hilo kutokea Majeruhi hao walipelekwa hospital na kupatiwa matibabu na hali zao zinaendelea vizuri.
Jeshi la Polisi linatoa rai kwa wananchi wanaoishi ndani ya Hifadhi na Pembezoni mwa Hifadhi hiyo ya Katavi kuondoka kwenye Maeneo hayo ili kuepusha changamoto za kushambuliwa na Wanyama kama Tembo ambao mara kadhaa hutoka katika Maeneo ya Hifadhi kutafuta Malisho.