WAKESHA SHAMBANI KWA KUHOFIA VIBOKO KUMALIZA MAZAO YAO

Madiwani wa Manispaa ya Mpanda wakiwa kwenye kikao Cha Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Manispaa ya Mpanda.


Na  Walter  Mguluchuma .

   Katavi.

Diwani wa Kata ya Mwamkulu Halmashauri ya Manispaa ya Mpanda Mkoani Katavi Kalipi Katani  amefikisha kilio cha wananchi wa Kata yake mbele ya kikao cha Baraza la Madiwani wa Manispaa ya Mpanda juu ya wananchi wake kukesha kwenye mashamba wakilinda mazao yao wakihofia kumalizwa na  wanyama aina ya Kiboko ambao wamekuwa tishio kwenye Kata ya Mwamkulu 

Diwani Kalipi alifikisha kilio hicho mbele ya Kikao cha Baraza la Madiwani wa Manispaa ya Mpanda kilichofanyika jana kwenye Ukumbi wa mikutano  wa Manispaa ya Mpanda  uliopo Mtaa wa Ilembo na Kikao hicho kiliongozwa  na Meya wa Manispaa ya Mpanda Haidary Sumry.

Alisema wananchi wamehama kwenye nyumba zao na kuacha kulala ndani ya nyumba  na badala yake  wamekuwa wakikesha kwenye mashamba hasa ya mbunga wakilinda mazao yao wakihofia kuliwa na kiboko ambao wamekuwa wakizagaa na kuwa tishio kwa wananchi .

Kalipi amebainisha kuwa hadi sasa zaidi ya ekari 20 za mazao yameliwa na kiboko  ambao wamekuwa wakitembea usiku kwenye mbuga za mpunga za wakulima.

Diwani wa Kata ya Mwamkulu Halmashauri ya Manispaa ya Mpanda Kalipi Katani akiwasilisha kilio cha wananchi wa Kata yake juu ya kulala kwenye mashamba yao wakihofia mazao  kuliwa na mnyama Kiboko ambao wamekuwa tishio kwenye Kata hiyo na hadi sasa zaidi ya ekali 20 za mazao zimeharibiwa na viboko(Picha na Walter MguIuchuma)


Alisema watu wamejenga nyumba kwa ajili ya kuishi na kulala  sasa nyumba hizo zimekuwa zikilala wazi  kutokana na wenye nyumba hizo  kulala kwenye mashamba yao wakiyalinda dhidi mnyama kiboko.

Aliomba Idara husika ya  Maliasili  kufanya utaratibu wa kuwadhibiti viboko hao  kabla ya kuleta madhara makubwa kwa wakazi wa Kata hiyo ambao wanaishi kwa kuhofia wanyama hao  aina ya viboko .

Meya wa Manispaa ya Mpanda Haidary Sumry alisema kuwa tatizo hilo la viboko kuvamia kwenye makazi ya watu na kuharibu mazao lipo pia kwenye Kata yake ya Makanyagio  hivyo ni vema  maeneo yote yenye matatizo hayo yakatambulika.

Nae Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Mpanda Sofia  Kumbuli  alisema kuwa swala hilo la  viboko watalifikisha Idara ya  Maliasili ya Halmashauri ya Nsimbo  ili kuwaomba wafanye operesheni ya kuwaondoa wanyama hao.

Manispaa ya Mpanda haina Idara ya Maliasili ndio maana wanalazimika kuomba msaada kwenye  Halmashauri ya jirani ya Nsimbo .

  

Search This Blog

CHAGUA HABARI

Pages