Jeshi la Polisi Mkoa wa Katavi linamshikilia Mzee mmoja aliyefahamika kwa jina la Simbuka Makande (62) Mganga wa kienyeji mkazi wa Kijiji cha Magengase Mkoa wa Tabora kwa tuhuma za kumbaka mwanamke (32) Mfanyabiashara wa madini ya dhahabu Mkazi wa Kijiji cha Katuma Wilaya ya Tanganyika Mkoa wa Katavi baada ya kumrubuni kuwa atamsafishia nyota ya kupata mali.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Katavi ACP Ali Makame Hamad amewaambia Waandishi wa Habari kuwa Mganga huyo wa Kienyeji alikuwa ametokea Mkoani Tabora na kufikia katika Kijiji hicho cha Katuma na kukodi chumba kwenye nyumba ya kulala wageni inayoitwa Bunga .
Ambapo mhanga wa tukio hilo nae alikuwa amefikia kwenye nyumba hiyo ya kulala wageni huku akiwa anaendelea kufanya biashara yake ya madini ya dhahabu yanayochimbwa kwenye Kijiji hicho cha Katuma .
Kamanda Makame aliendelea kueleza kuwa ndipo mwanamke huyo alipokutana na Mganga Makande na alimweleza mwanamke huyo kuwa anao uwezo wa kuwasafishia watu nyota zao ili waweze kupata mafanikio kwenye shughuli zao na moja ya masharti yake ni kufanya nae mapenzi .
Alisema ndipo Mganga huyo alimrubuni mhanga na kufanya nae mapenzi kwa nyakati tofauti tofauti na pia mhanga aliweza kumpatia mganga kiasi cha shilingi milioni moja na elfu sitini .
Amebainisha kuwa Mganga huyo pia anatuhumiwa kufanya vitendo hivyo kwa watu watatu Mkoani Katavi na kujichukulia kwa watu hao kiasi cha shilingi milioni nne na laki sita.
Amekuwa pia akiwatapeli watu hao kuwa amesha wasaidia viongozi wengi kupata mafanikio na kisha kufanya nao mapenzi kwa kuwarubuni kuwa atawasaidia kupata mafanikio kama hayo katika biashara zao na maisha kwa ujumla .
Kamanda Makame amesema mtuhumiwa amekamatwa na enaendelea kuhojiwa na Jeshi la Polisi na mara upelelezi utakapo kamilika atafikishwa Mahakamani kujibu tuhuma zinazomkabili.