Kamanda wa Polisi Mkoa wa Katavi ACP Ali Makame Hamad akitoa taarifa ya matukio mbalimbali yaliyojitokeza Katika Mkoa wa Katavi mbele ya Waandishi wa habari(Picha na Walter MguIuchuma) |
Mtu mmoja aliyefahamika kwa jina la Machia Mbasa (General)miaka 65 Mkazi wa Kijiji cha Lwafe Wilaya ya Tanganyika Mkoa wa Katavi anashikiliwa na Jeshi la Polisi kwa tuhuma za kupanga njama za kumuua Mabula Ntemange(37) kwa kumtuhumu kuwa na mahusiano ya kimapenzi na mke wake mdogo wakati yeye alipokuwa gerezani .
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Katavi Ally Hamad Makame amethibitisha kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo na Jeshi la Polisi kufutia taarifa zilizowafikia za mtuhumiwa kutekeleza mauaji hayo yaliyosababishwa na wivu wa kimapenzi .
Kamanda Makame alisema pia mtuhumiwa alikuwa akimtuhumu Mabula Ntemange kuchukua kodi kwenye vibanda vyake ya biashara alivyovijenga eneo hilo la Lwafe na kwenda kustarehe na mke wake huyo mdogo wakati yeye akiwa kwenye gereza la mahabusu Mpanda Mjini kwa tuhuma za mauaji.
"...baada ya Jeshi la Polisi Mkoa wa Katavi kupata taarifa hizo walichukua hatua za haraka na kufanikiwa kuzuia jaribio hilo la mauaji kwa kumkamata mtuhumiwa Mbasa kabla haja tekeleza mauaji hayo"alibainisha Kamanda Makame.
Hivyo mtuhumiwa amekamatwa na kufikishwa kituo cha Polisi kwa ajili ya mahojiano zaidi juu ya kutaka kutekeleza kitendo hicho cha kukatisha uhai wa binadamu mwenzake ambapo kisheria ni kosa kuuwa kwani kila mtu anahaki ya kuishi.
Baada ya kuhojiwa mtuhumiwa alikiri kupanga njama za kutaka kufanya hivyo kutokana na hasira ya jirani yake huyo kuwa na mahusiano ya kimapenzi na mke wake mdogo anayempenda wakati yeye akiwa anasota mahabusu.
Kamanda Makame amebaisha kuwa mtuhumiwa huyo alikuwa amewakodi wauaji wawili kutoka Kaliua Mkoani Tabora na baada ya wauaji hao kufika Mjini Mpanda walipokelewa na mtuhumiwa na kisha walihifadhiwa kwa ajili ya kusubiri kutekeleza mauaji hayo.
Mbali ya kupanga mauaji hayo mtuhumia Machia Mbasa amekuwa pia akituma ujumbe wa vitisho vya mauaji kwa watu wawili ambao ni Charles Lugembe na Dogani Malima wote wakazi wa Kijiji cha Mwamkulu Manispaa ya Mpanda .
Mtuhumiwa bado anaendelea kuhojiwa na Jeshi la Polisi ili kubaini mtandao mzima anaoshirikiana nao kutekeleza vitendo vya mauaji na mara baada ya upelelezi kukamilika atafikishwa Mahakamani kujibu tuhuma zinazo mkabili.