Na Walter MguIuchuma,Katavi
Jeshi la Polisi Mkoa wa Katavi limefanikiwa kumkamata mtuhumiwa maarufu wa wizi wa pikipiki anaefahamika kwa jina la Laurenti Lazaro (61) Mkazi wa Kanoge Wilaya ya Mpanda akiwa ameiba pikipiki tano za watu tofauti tofauti.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Katavi Ally Hamad Makame amewaambia Waandishi wa Habari ofisini kwake mtuhumiwa huyo alikamatwa hapo juzi majira ya saa kumi jioni huko katika Mtaa wa Msufini Kata ya Uwanja wa Ndege Manispaa ya Mpanda.
Kabla ya kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo Jeshi la Polisi Mkoa wa Katavi waliandaa msako mkali wa kupambana na uhalifu na waliweza kufanikiwa kumkamata mtuhumiwa huyo akiwa na pikipiki ya wizi yenye Namba za usajiri MC 915 CDV aina ya HONLG yenye rangi nyekundu.
Kamanda Ally Makame alisema baada ya mtuhumiwa huyo kukamatwa na kufanyiwa mahojiano ya kina alikiri kuwa aliiba pikipiki nyingine nne kwenye maeneo tofauti tofauti ya Mkoa wa Katavi na aliweza kwenda kuzionyesha pikipiki hizo.
Ambapo katika msako huo walifanikiwa kupata pikipiki hizo nne na kufanya jumla ya pikipiki tano alizokuwa ameiba mtuhumiwa huyo zenye Namba za usajiri MC,445 AAA ina ya SANLG rangi nyekundu , MC 553 ADM aina ya SANLG rangi nyekundu,MC 468 CUC aina ya SINOREY na MC 802 CQJ aina ya SYNOTEY.
Makame alieleza kuwa mtuhumiwa huyo alikuwa akiiba kwa kutumia mbinu ya kutembea na funguo bandia ambazo ndizo alikuwa akizitumia kuibia pikipiki zinazokuwa zimepakiwa kwenye maeneo mbalimbali na wamiliki wa pikipiki hizo.
Mtuhumiwa bado anaendelea kuhojiwa ili kuweza kuwapata washiriki wake wanao shirikiana nae katika kufanya wizi huo wa pikipiki na mara baada ya upelelezi kukamilika mshitakiwa atafikishwa mahakamani kujibu tuhuma zinazo mkabili.