Na George Mwigulu,Mlele.
Zaidi ya Wananchi 23,000 wa Kata ya Ilunde Halmashauri ya Wilaya ya Mlele Mkoa wa Katavi wataepukana na adhaa ya kutembea umbali mrefu zaidi ya Km 60 kufuata huduma ya afya Kituo cha Afya Inyonga baada ya kuwekewa jiwe la msingi kituo chao cha Afya Ilunde.
Jengo la kituo cha afya Ilunde halmashauri ya wilaya ya Mlele Mkoa wa Katavi ambalo litasaidia kwenye utoaji wa huduma ya afya- (Picha na Erenest Kibada) |
Hali hiyo imewafanya wananchi kuishukuru serikali kwa kuwakumbuka wananchi na kuwaletea fedha kiasi cha silingi milioni 792,100,000 kwa ajili ya ujenzi wa majengo katika kituo hicho ambacho kimewekewa jiwe la msingi na Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru kitaifa mwaka 2022,Sahili Geraruma.
Wakizungumza wananchi hao wameishukuru Serikali kwa kazi nzuri ya iliyofanyika ya kuwapelekea fedha za ujenzi wa miundombinu ya afya.
Martin Mgoloka,Mkazi wa Kata ya Ilunde ameishukuru serikali kwa jinsi walivyowaheshimisha wananchi hao, ambao walikuwa wakijiona kama vile wametengwa na serikali ambapo kwa sasa nao wanaonekana kuwa ni watanzania.
Mgoloka amesema fedha zilizoletwa kiasi cha Mil 792.1 zimesaidia kuboresha majengo ya kituo hicho cha afya kilichokuwa na majengo machache na huduma zilikuwa hazijaanza kutolewa sasa.
Dkt Leticia Sebastin,Mganga Mfawidhi wa kituo cha Afya Ilunde akisoma taarifa ya maendeleo ya ujenzi wa majengo ya kituo kwa Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru kitaifa mwaka 2022,Sahili Geraruma amesema mradi huo ni mwendelezo wa ukamilishaji wa majengo muhimu ya kituo cha afya kilichoanza mwaka wa fedha 2018/2019.
Mganga mfawidhi huyo amesema mradi huo umehusisha ujenzi wa jengo la wagonjwa wa nje,Sehemu ya kuchomea taka,Shimo la kutupia kondo la nyuma na Jengo la kufulia ambayo yaliletewa kiasi cha Mil 250,000/=
Ujenzi wa jengo la wagonjwa wa ndani,,Jengo la Baba ,Mama na Mtoto pamoja na Jengo la Mionzi lililochukua kiasi cha shilingi 400,000,000/=
Aidha ujenzi wa matundu matatu ya vyoo,Jengo la mfumo wa maji na ujenzi wa tanki la maji yenye ujazo wa lita 30,000.
Vilevile alisema kuwa kukamilika kwa kituo hicho ,kutaboresha huduma za Afya kwa wakazi wa kata ya Ilunde wakiwa ni akina mama wajawazito na watoto chini ya umri wa miaka mitano.