Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Mwanamvua Mrindoko. |
Na. Zillipa Joseph, Katavi.
Ikiwa imebaki takriban wiki moja ili kuanza kwa muhula mpya wa masomo kwa shule za msingi na sekondari hapo Januari 8 mwaka 2024; mkoa wa Katavi unatarajia kuchukua jumla ya wanafunzi 42,974 wa darasa la awali na wanafunzi 39,326 wa darasa la kwanza.
Mwonekano wa baadhi ya madarasa ya awali. |
Akitoa taarifa hiyo kwa vyombo vya habari Mkuu wa Mkoa wa
Katavi Bi. Mwanamvua Mrindoko amesema kwa kipindi cha Januari hadi Disemba 2023
mkoa huo ulipokea kiasi cha shilingi bilioni 19.4 kwa ajili ya kuboresha
miundombinu katika shule za msingi na sekondari.
Mkuu huyo wa mkoa wa Katavi ameongeza kuwa katika fedha
hizo wameweza kujenga shule mpya kumi za msingi na kuongeza vyumba vya madarasa
katika baadhi ya shule.
Aliongeza kuwa madarasa hayo yataweza kupunguza msongamano
wa wanafunzi na kuwapokea wanafunzi wapya wa madarasa ya awali na darasa la
kwanza.
Aidha Bi. Mrindoko amewaagiza wazazi wenye watoto wa
kuanzia umri wa chini ya miaka mitano kuhakikisha wanawaandikisha watoto shule.
‘Kwa wazazi au walezi watakaokiuka agizo hili
tutawachukulia hatua kwani sheria zipo’ amesema.
Akizungumza kwa niaba ya Afisa Elimu mkoa wa Katavi, Mratibu wa Elimu mkoa bwana George Mtawa amesema lengo ni kuandikisha wanafunzi 42,974 wa darasa la awali na mpaka sasa wameandikisha wanafunzi 15,189 sawa na asilimia 35.34%.
Kwa upande wa darasa la kwanza amesema lengo ni
kuandikisha wanafunzi 39,326 na wameandikisha wanafunzi 23,051 sawa na asilimia
58.62%.
Pia ametoa wito kwa wazazi na walezi wawaandikishe watoto
shule.
Amesema serikali imekwishajipanga kuwapokea wanafunzi
wapya, hivyo ni wajibu wa wazazi kuhakikisha wanakamilisha mahitaji ya muhimu
ikiwemo sare za shule na madaftari.
Kwa upande wao baadhi ya wazazi ambao hawajawaandikisha
watoto shule (majina tunayahifadhi) waliofikiwa na mwandishi wetu wamekuwa na
sababu kadhaa ikiwemo kukosa fedha za sare na wengine wakidai hawana vyeti vya
kuzaliwa vya watoto.
‘Mimi sijampeleka mtoto nasubiri baba yake atoke shamba ndio
tukamwandikishe maana nikienda mwenyewe watasema ni mtoto wa mzazi mmoja’
amesema mama mmoja mkazi wa Mpanda.
Aidha kwa wazazi waliowaandikisha watoto kuingia madarasa
ya awali wengi wao wamefurahia ubora wa miundombinu iliyojengwa na serikali na
hata kufikia kufananisha madarasa yake na yale yanayopatikaana katika shule za
binafsi za kulipia.
Kwa upande wa walimu wakuu wa shule tofauti za msingi;
walipoulizwa kuhusu wanafunzi kuhudhuria na nguo za nyumbani wako waliokubali
watoto wafike bila hata ya sare za shule na wako waliopinga.
‘Wewe fikiria ndugu mwandishi serikali imejenga madarasa
mazuri kama haya ya awali halafu wewe
ulete mtoto wako hapa amevaa yebo! Wawanulie viatu’ amesema mwalimu mkuu
mwingine.
‘Inapendeza mtoto akija shule awe amekamilika, na hata
akipita njiani anafahamika ni mwanafunzi, lakini kutokana na hali zetu
kutofautiana inabidi kuwaruhusu hata wasio na sare kuja shule watanunua
polepole’ amesema mwalimu mwingine.